WAKAZI ZAIDI YA 1000 KUONDOKANA NA KERO YA MAJI MISUNGWI MKAONI MWANZA

Kero ya uhaba wa maji iliyokuwa ikiwakabili wananchi zaidi ya 1000 wa vitongoji vitano vya Kijiji cha Kasololo wilayani Misungwi mkoani Mwanza na kusababisha ndoa nyingi kuvunjika pamoja na migogoro kwenye familia, imetatuliwa baada ya Taasisi ya The Desk & Chair Foundation kuchimba na kujenga visima saba.

Mwenyekiti wa The Desk & Chair Foundation tawi la Tanzania Sibtain Meghjee akikabidhi visima hivyo vilivyogharimu sh 21 milioni alisema walisitisha ujenzi wa Msikiti (nyumba ya ibada ) ili watatue kero ya maji kwa kuwapa wananchi huduma ya maji itakayowanufaisha watu zaidi ya 1200 kwa matumizi ya kibinadamu.

Alisema visima vimekabidhiwa ili kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Bi. Fatma AS. mjukuu wa Mtume Mohamed S.A.W.ambaye alifanya kazi kubwa ya kusaidia jamii lakini pia miradi ya kijamii inayofadhiliwa na waumini wa madhahebu ya Shia Ithna Asheri, kwenye maadhimisho hayo ilikabidhiwa huko Kwimba Mwanza na Kondoa mkoani Dodoma na maeneo mengine nchini.

“Dini ya Kiislamu licha ya kupakaziwa mambo ya ovyo na kuhusishwa na ugaidi ni nzuri na haya yanayofanywa na The Desk & Chair Foundation ndiyo uislamu wenyewe.Tumewapunguzia kero ya maji wananchi wa Kasololo na siri ya kudumu kwa visima hivi matunzo ni muhimu lakini pia tengeni maeneo yasiyo na migogoro kwa ujenzi wa maombi mapya ya visima,”alisema Sibtain.

Wakizungumza jana baada ya kukabidhiwa visima hivyo saba vya maji safi na salama vilivyochimbwa katika vitongoji vitano vya vya Isuka, Bugumo, Mwashileko,Iwelimo na Kasololo baadhi ya wananchi walisema tatizo hilo la ukosefu wa maji lilikuwa linawakabili kwa muda mrefu litapungua ingawa bado changamoto ipo.

Petro Mbogo mkazi wa kitongoji cha Iwelimo kilichopata visima vitatu alisema kero ya maji ilisababisha migongano kwenye jamii, migogoro katika familia pamoja na ndoa nyingi kuvunjika kutokana na akina mama kukesha wakisubiri kuteka maji usiku kwenye vyanzo vya asili ambavyo hukauka wakati wa kiangazi.

“Maji yalikuwa kero kwa miaka mingi katika kijiji chetu na wakati wa kiangazi tulisafiri umbali wa km 5 kwenda kuchota maji ziwani.Wanawake walikuwa wakisumbuka mno kupata maji, ndoa nyingi zilivunjika, kulizuka migongano na migogoro kwenye familia sababu ya maji,”alisema Mbogo.
Alisema kupatikana kwa visima hivyo sasa kutawapa wanawake fursa na muda wa kufanya shuguli za uzalishaji pamoja na maendeleo tofauti na zamani ambapo walipoteza muda mwingi wakitafuta maji kwa matumizi ya familia zao na kushindwa kuzalisha.

Naye Mariamu Jeremiah wa kitongoji cha Bugumo alisema visima hivyo vitakidhi mahitaji ya wananchi wa vitongoji vya kijiji hicho ambao awali walifikia hatua ya kupigana wakigombea kuchota maji kutoka kwenye visima vya asili kwa kulowa maji (kuchota kwa kutumia kamba) huku wakilazimika kuwaacha waume zao wamelala kwenda kutafuta maji.

“Mungu amesikia kilio chetu cha maji japo pump ni nzito kwa watu wa umri mkubwa,tunashukuru kwa msaada huu wa visima vya maji, maana hatukuwa tunaoga wala kufua nguo za waume zetu, ndoa zilivunjika wanawake wengine walipigwa na waume zao kwa kuchelewa sababu ya maji,watoto walikatishwa masomo,walikuwa hawanawi nyuso,”alisema Bi. Jeremiah.

Alidai walilazimika kuyafuata maji ziwani umbali wa maili 5 kutokana na kuambulia ndoo moja kwenye kisima wakichukua muda wa saa 8 kuipata huku ndoo moja ya ujazo wa lita 18 wakiuziwa sh.500 hali ambayo kwa wananchi wasiokuwa na ajira yalikuwa ni mateso kumudu gharama za maji kwa familia.

Kwa mujibu wa wakazi wa kitongoji cha Iwelimo Susan Fustine,Rahel Yuda,Shoma Motomkali na Regina Joseph licha ya kusogezewa karibu huduma hiyo bado wanakabiliwa na adha kubwa ya maji na hivyo waongezewe visima vingine huku Mwalimu Mkuu msaidizi wa Shule ya Sekondari Kasololo Rahim Ayoub akieleza kuwa walimu na wanafunzi watayatumia maji hayo kwa mahitaji ya kibinadamu na kumwagilia miti ili kuboresha na kutunza mazingira ya shule.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Kasololo Ruben Masasi licha ya kushukuru kwa msaada huo ambao haukutegemewa alidai umeondoa migogoro kwenye familia zilizokumbwa na kadhia hiyo na kunusuru ndoa zisiendelee kuvunjika lakini kutokanana idadi ya ongezeko la watu,mahitaji yataongezeka na kuomba wasaidiwe visima vingine.


Mwenyekiti wa The Desk & Chair Foundation tawi la Tanzania Sibtain Meghjee akimtwisha ndoo ya maji milembe Kuhamwa, Mwenyekiti wa Kiyongoji cha Mwashileko katika Kijiji cha Kasololo wilayani Misungwi Mwanza, ikiwa ni ishara ya kukabidhi kisima cha maji safi na salama kati ya saba vilivyochimbwa na taasisi hiyo kwa gharama ya sh. 21 milioni.

Mwenyekiti wa The Desk & Chair Foundation Sibatain Meghjee (kushoto nyuma ya pump ya maji) akizungumza na wananchi baadhi wa Kijiji cha Kasololo katika Wilaya ya Misungwi baada ya kuwakabidhi moja ya visima vilivyochimbwa na taasisi hiyo hivi karibuni.

Wananchi wakimsikiliza mfadhili aliyechimba visima vya maji Sibatin Meghjee Mwenyekiti The Desk & Chair Foundation ili kukabiliana na kero ya maji kijijini Kasololo Misungwi hivi karibuni.

Share on Google Plus

About Unknown

0 comments:

Post a Comment