MAKONDA AWAFUTA KAZI MAAFISA ELIMU 12, BAA, NYUMBA ZA WAGENI KUVUNJWA


Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mheshimiwa Paul Makonda leo amefanya mkutano na watendaji wa sekta ya elimu wakiwemo Maafisa elimu ngazi zote na Wakuu wa Shule za Msingi na Sekondari kwa lengo la kujadili namna bora ya kuboresha ufaulu kwa wanafunzi na uboreshaji wa Sekta ya Elimu.

Katika Mkutano huo Makonda ametoa fursa kwa wakuu wa Shule na Maafisa Elimu kueleza changamoto na sababu zinazosababisha Wanafunzi kutofanya vizuri katika masomo ambapo baada ya kusikiliza kero hizo ameahidi kuzifanyia kazi kwa kipindi cha muda mfupi.

Miongoni mwa mambo ambayo Makonda ameahidi kuyatekeleza kwa muda mfupi ni pamoja na kuhakikisha shule zote zinaunganishwa na huduma ya Umeme, Vyoo vya walimu na wanafunzi,Ofisi za walimu na Samani zake pamoja na kutoa mabati kwa shule zenye mabati chakavu.

Akizungumza na watendaji hao Makonda amesema kuwa amedhamiria kuboresha sekta ya Elimu kwa kuhakikisha anamaliza kero zote zinazokabili sekta hiyo ili walimu waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi ili kuongeza ufaulu na kuufanya Mkoa wa Dar es salaam kutoa elimu bora.

“Nataka tumalize kero zinazowakabili ili nyie muweze kutekeleza majukumu yenu ya kutoa elimu bora, sitaki mpate sababu ya kuwakwamisha, na kwakweli jisikie vibaya shule yako inapofanya vibaya, nachotaka mjikite kwenye nafasi yenu kama mimi ninavyojikita kwenye nafasi yangu” Amesema Makonda
Kuhusu changamoto ya upungufu wa walimu kwa baadhi ya shule, *Mh. Makonda* amewaagiza maafisa elimu kutatua changamoto hiyo kutokana na kuwepo kwa baadhi ya shule zenye walimu wengi huku nyingine zikiwa na wachache.

Hata hivyo ameahidi *kuwapatia usafiri wa Pikipiki Maafisa Elimu wa Kata* ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kuwaongezea usafiri wa magari kwa wadhibiti wakuu wa ubovu wa shule kwenye Manispaa ya Ilala.

Pamoja na yote Mheshimiwa Makonda amemuagiza Afisa Elimu wa Mkoa kuwavua madaraka Maafisa elimu wa kata 12 kutokana na matumizi mabaya ya madaraka na fedha za elimu kiasi cha Shilingi laki mbili na nusu kila mwezi ambazo wanapatiwa kwaajili ya shughuli za Elimu lakini hao wamekuwa wakizitumia kununua Vipodozi na Mavazi badala ya elimu.
Aidha Makonda amewaagiza walimu wakuu kuandika maelezo ya nini kinachokwamisha shule yake hadi kushindwa kufanya vizuri pamoja na mapendekezo ya nini kifanyike ili kuongeza ufaulu kisha kuwasilisha kwa Afisa Elimu ndani ya siku saba kuanzia sasa.

Katika hatua nyingine Makonda ametoa siku 20 kwa Wakuu wa shule kuhakikisha Bar na nyumba za Wageni(Guest houses) zilizojengwa kwenye maeneo ya shule zinavunjwa mara moja kutokana na usumbufu wanaosababisha kwa wanafunzi muda wa masomo. Bar na Nyumba hizo ni matokeo ya usimamizi mbovu wa watendaji ambao walishiriki kwa namna moja au nyingine kuuza au kukodisha maeneo yaliyotengwa na serikali kwa ajiri ya shule kwa watu walioweka na kufanya biashara hizo na kuathiri lengo la utoaji elimu bora kwa watoto wanaotegemea shule hizo


Share on Google Plus

About Unknown

0 comments:

Post a Comment