MALAWI IMETANGAZA KUJIONDOA KWENYE MICHUANO YA CHAN NA AFCON

Malawi imetangaza kujiondoa kwenye michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika 2019 pamoja na michuano ya Ubingwa Afrika kwa wachezaji wa ligi za nyumbani ya 2018. Maamuzi hayo yamechukuliwa kutokana na matatizo ya kifedha pamoja na kukosa kocha wa timu ya taifa. Shirikisho la Soka la Malawi lilitoa taarifa baada ya kunyimwa idhini ya kumwajiri kocha kutoka nje na serikali ya nchi hiyo.
Shirikisho la nchi hiyo lilitaka kumwajiri mkufunzi kutoka nje ya nchi ambaye angelipwa mshahara kwa ubia wa nusu nusu kati ya shirika hilo na serikali. Baada ya mashauriano ya miezi kadhaa, serikali kupitia Wizara ya Michezo ilikataa pendekezo la shirikisho hilo kwa misingi ya kifedha na ndipo kama tendaji ya shirikisho hilo ilipofikia uamuzi wa kujiondoa kwenye michuano hiyo ya ubingwa wa bara la Afrika.
Timu ya taifa ya Malawi itaondoka rasmi kutoka kwa CHAN kufikia 31 Machi na kutoka AFCON kufikia 30 Aprili. Timu ya taifa ya Malawi ilikuwa imepangiwa kucheza dhidi ya Madagascar mechi yao ya kwanza ya kufuzu kwa CHAN 2018, michuano ambayo imepangiwa kuanza Aprili.
Kadhalika, walipangiwa kucheza nyumbani mechi yao ya kwanza ya kufuzu kwa AFCON 2019 na mshindi wa mechi kati ya Comoro na Mauritius tarehe 13 Juni.
Malawi imekuwa bila mkufunzi wa timu ya taifa tangu Septemba 2016 raia wa Burundi Nsanzurwimo Ramadhan alipowaongoza kwa mechi moja ambayo walishinda 1-0 dhidi ya Swaziland mechi ya kufuzu kwa AFCON alikuwa amechukua usukani baada ya kufutwa kwa Ernest Mtawali Julai mwaka huo.


Share on Google Plus

About Unknown

0 comments:

Post a Comment