Katibu Mkuu wa chama cha wananchi
CUF, Maalim Seif Sharif Hamad amewasilisha barua kwa Spika wa Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Jon Ndugai akimtaarifu kuwa Baraza Kuu la Uongozi la
Taifa la CUF limewasimamisha uanachama wanachama wawili wa chama hicho ambao ni
Naibu Katibu Mkuu wa CUF, Magdalena Sakaya (Mbunge wa Kaliua) na Maftaha
Nachuma (Mbunge wa Mtwara Mjini) uamuzi uliofikiwa kutokana na wajumbe wa
mkutano huo kupiga kura za siri na kuamua kuwavua uanachama, hivyo amemuomba
Spika Ndugai afanye utaratibu wa kuwavua ubunge kwa kuwa si wanachama halali wa
chama hicho.
Maalim Seif Sharif Hamad |
Baada ya barua hiyo, Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji
Francis Mutungi amejibu barua ya Maalim Seif kwa kueleza kutomtambua yeye kama
Katibu Mkuu wa CUF kwakuwa barua kutoka chama hicho ilisema kuwa nafasi ya
Katibu Mkuu wa chama inakaimiwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa
haijapokea barua nyingine kutoka chama hicho ikionesha kumrejeshea Maalim Seif
mamlaka yake.
Pia Jaji Mutungi amekataa matokeo ya kikao hicho kilichoitishwa
na Maalim Seif kwakuwa kikao hicho kilitakiwa kiwe chini ya mtu mwenye dhamana
ya Katibu Mkuu wa chama (Magdalena Sakaya) au Mwenyekiti wa CUF (ambaye ni
Profesa Ibrahim Lipumba) na Jaji Mutungi akamkumbusha Maalim Seif arejee Katiba
ya CUF ibara ya 91(c) inayotaka vikao vyote vya Baraza Kuu la chama hicho
viongozwe na Mwenyekiti wa chama.
0 comments:
Post a Comment