SERIKALI KUGHARAMIA MATIBABU YA TUNDU LISSU

Serikali imesema ipo tayari kugharamia matibabu ya Mbunge wa Jimbo  la Singida Mashariki  Tundu Antiphas Lissu  ambaye kwa sasa hivi yupo Jijini Nairobi kwa matibabu kufuatiwa shambulio alilolipata Septemba 7, mwaka huu Mkoani Dodoma.

Hayo yamesemwa Jijini Tanga na Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati akiongea na waandishi wa habari kwenye ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo.

Waziri Ummy Mwalimu alisisitiza kwa kusema kuwa Serikali inasubiri kupata maombi kutoka kwa familia ya mgonjwa ikiambatana na taarifa rasmi kutoka kwa  madaktari kuhusu mahitaji ya matibabu zaidi  ya mgonjwa ”Serikali ipo tayari  kugharamia matibabu  zaidi ya Mhe.Lissu popote Duniani” alisema Waziri Ummy. Aliongeza kwa kusema, akiwa kama Mtanzania na Mbunge,Serikali inayo wajibu wa kugharamia matibabu yake hadi apone ili aweze kuendelea na kazi ya kuwahudumia Watanzania na wana Singida Mashariki.

Aidha, Serikali imeshangazwa na dhana ya kuchangishana kwa ajili ya matibabu ya Mhe. Lissu, kwani kwa kufanya hivyo kunaweza kutokea matapeli watakaochangisha Watanzania fedha kwa madai kwamba Mbunge huyo amekosa hela za matibabu.

Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia, Wazee na Watoto anawashukuru Madaktari na watoa huduma wote wa Hospitali ya Rufaa Dodoma kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya katika kuokoa maisha ya Mhe.Lissu na kumtakia apate nafuu haraka.
Share on Google Plus

About Unknown

0 comments:

Post a Comment